Wednesday 15 October 2014


LICHA ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Kinondoni kupitia kwa kamanda wake, Camillius Wambura kutumia nguvu kubwa kukanusha kwamba, hakuna matukio ya utekaji wa watoto wadogo, hasa wanafunzi, lakini matukio hayo YAPO!! 
Mama aliyempoteza mwanaye akilia kwa uchungu.
UWAZI LINA CHA KUSHIKA
Ili kuliwekea ushahidi suala hilo, Uwazi lina cha kushika mkononi kufuatia wiki iliyopita, wanafunzi wawili wa shule za  msingi wilayani Kinondoni ambako Kamanda Wambura anasimamia jeshi lake walipotea na baadaye kuokotwa wakiwa wameuawa. 


MATUKIO YENYEWE
Wanafunzi hao ambao miili yao iliokotwa, mmoja akiwa amenyofolewa sehemu za siri ni Glory William (7), mwanafunzi wa darasa la kwanza Shule ya Msingi Msingwa na Joshua Nicolas (12) wa darasa la saba katika Shule ya Msingi Temboni, zote ni wilayani Kinondoni kwa Kamanda Wambura.

 
Mama mwingine aliyefiwa akilia kwa uchungu.
MAMA WA GLORY ASIMULIA KWA MACHOZI
Akizungumza na mwandishi wa habari hii siku ya tukio, mama mzazi wa Glory, Faminian Gabriel alisema:
“Jamani wanaposema hakuna utekaji wa watoto huku sisi wazazi tunalia, si sawa! Nakumbuka siku ya jana (Ijumaa) saa kumi jioni mwanangu Glory alirudi toka shule, nilimkumbatia kwa upendo kisha nikamuacha nyumba ya jirani na mfanyakazi wa ndani.

“Mimi niliondoka kwenda kwenye kazi fulani. Niliporudi sikumkuta Glory nyumbani, nilipoulizia nikaambiwa alikuwa na kijana mmoja,” alisema mama huyo.
 
Waombolezaji wakiubeba mwili wa mmmoja wa watoto waliuwawa.
AFIKA KWA MJUMBE
Haikuwa kawaida ya Glory kuwa mbali na nyumbani jambo ambalo lilinitia hofu. Ilibidi nikatoe taarifa kwa mjumbe ambaye tulisaidiana naye kumtafuta lakini bila mafanikio.” 


SERIKALI ZA MTAA WAAMBIWA, WASHANGAA
Baadaye pia nilikwenda kutoa taarifa kwenye ofisi za serikali za mtaa lakini mtoto hakuonekana na wao wakashangaa mazingira ya upoteaji wake.

 
Baadhi ya waombolezaji wakiendelea na mazishi.
GIZA HADI KUNAKUCHA MTOTO HAJARUDI
Mama Glory aliendelea kusema kuwa alikaa macho hadi asubuhi bila kumuona binti yake. Wakati anajiandaa kwenda kutoa taarifa kituo cha polisi sasa, akapata taarifa kwamba kuna mwili wa mtoto umeokotwa mahali.

“Baada ya kupewa taarifa hizo, majirani walifuatana na mimi na ndugu zangu hadi eneo la tukio na walipoukagua mwili ukabainika ni mwanangu,” alisema mama huyo huku akilia. 

MWILI ULIVYOKUTWA, INAUMA!
Inaelezwa kwamba, baadhi ya wananchi walipoukagua vizuri mwili huo walitokwa machozi kufuatia kubaini kuwa, hakuwa na sehemu za siri, pia kichwa chake kilionekana kupondwa na tofali, pengine ndilo lililosababisha kifo chake.

 
Baadhi wanafunzi wakiweka shada la mauwa kwenye kaburi la mtoto aliyeuawa.
KUANDAMANA HADI IKULU YA JK
Baadhi ya wazazi waliozungumza na Uwazi kwenye msiba wa mtoto Glory walisikika wakisema wanajipanga kufanya maandamano ya amani hadi Ikulu ya Rais Jakaya Kikwete kumlalamikia kuhusu kukithiri kwa matukio ya utekaji watotohuku jeshi la polisi likisema hakuna kitu kama hicho.  


ALIVYOSEMA MJUMBE
Akithibitisha habari hiyo, Mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa Saranga kulikotokea tukio, Samora Costino alisema mauaji ya mtoto huyo yana ushirikina ndani  yake na kwamba huyo ni mtoto wa pili kutekwa na kuuawa kikatili. 


TANGU MACHI TATIZO LIPO
Mjumbe huyo alisema mtoto Joshua yeye alitekwa Machi 18, mwaka huu akiwa anatoka shule, akauawa na maiti yake ikatupwa mtoni.

 
Hili ni kaburi la mmoja wa watoto waliouawa
BABA MZAZI WA JOSHUA AKUMBUKA MACHUNGU
Uwazi lilifanikiwa kuzungumza na baba mzazi wa Joshua, mzee Nicolas ambaye alikiri mwanaye huyo kutekwa akitoka shule na kuuawa. Alisema:

“Siku hiyo ya tukio mwanangu hakurudi nyumbani kutoka shuleni. Tulimtafuta bila mafanikio hadi kesho yake alipookotwa kwenye mto huko Tabata Mawenzi akiwa ana alama shingoni kuonesha kwamba alipigwa na kunyongwa. 

“Hata hivyo, muuaji alijulikana lakini cha kushangaza hajakamatwa hadi leo. Pia nawashangaa polisi kwani hata taarifa ya uchunguzi wa kifo sijapewa jambo lililonifanya niamue kwenda Ofisi ya IGP (Ernest Mangu) ambapo kwa sasa mambo yanaendelea vizuri,” alisema mzee huyo.
 
Marehemu Glory William (7)(kulia)  akiwa na wenzake enzi za uhai wake.
KUMBUKUMBU
Siku za hivi karibuni jijini Dar es Salaam, watoto, hususan wa shule za msingi wamekuwa wakidaiwa kutekwa na watu wanaosemekana hutumia magari aina yaToyota Noah rangi nyeusi hali inayowafanya wazazi kuwa na hofu. 
Baadhi ya shule tayari zimeweka sheria kwamba, wazazi wasiwaache watoto wao kwenda shuleni wenyewe au kupelekwa na watu wasiowaamini.Katika gazeti hili toleo la wiki iliyopita, ukurasa wake wa mbele kulikuwa na habari kubwa yenye kichwa; UTEKAJI WATOTO WATIKISA DAR!
 
Marehemu Joshua Nicolaus Rubanzibwa enzi za uhai wake.
Katika habari hiyo, tukio moja la ajabu lilitokea Vingunguti, Ilala ambapo gari aina ya Noah lilivamia shuleni na kumteka mwanafunzi mmoja na kutaka kuondoka naye.Hata hivyo, mzazi mmoja alishuhudia kitendo hicho na kupiga kelele hadi watu hao wakamwachia mtoto huyo. 

Kesho yake, Noah lingine jeusi lilifika kwenye shule ya jirani na ya mtoto wa jana yake kwa lengo la kuzungumza na walimu kuhusu mikopo.Ikadaiwa kuwa, wazazi walipoliona Noah hilo jeusi walilipopoa mawe wakiamini ni lile la jana yake lilirudi tena. Ilibidi Polisi wa Kituo cha Buguruni waitwe kurejesha hali ya amani shuleni hapo

0 comments:

Post a Comment

Design by GG greggy| Blogger Theme by greggy - Premium Blogger Templates | NewBloggerThemes.com